
MWANA
Shikamoo wangu babu
Kukusalimu wajibu
‘Metuamuru wahabu
Heshima kuwapatia
BABU
Marahaba ya kijana
Habari za tangu jana
‘mefurahi kukuona
Kwako mi najivunia
MWANA
Za tangu Jana ni njema
Nami pia ni mzima
Sina panaponiuma
Namshukuru jalia
BABU
‘Mefurahi kusikia
Kuna mambo ainia
Nataka kukuambia
Nakusihi zingatia
MWANA
Mimi nimemakinika
Tayari kunufaika
Busara yako hakika
Mimi naiaminia
BABU
Kwanza jambo lilo aula
Muogope wako mola
Usiziache zote swala
Madhambini kajitia
Shikilia sana dini
Iwe thabiti imani
‘kiondoka duniani
Pema upate shukia
Pili hao marafiki
Wengine ni wanafiki
Wakifanya ufasiki
Siwaandame sikia
Na wengine ni wahuni
‘Takutia hasarani
Wakushushe na thamani
Mwishoni ukajutia
Kwa hiyo jiweke mbali
Uyafanye ya halali
Umridhishe jalali
Na wazazi wako pia
Rafiki wa kufuata
Ni yule aso matata
Vitabu huvikamata
Na bidii akatia
Na pia hiyo adabu
Ishikilie shababu
Utaziepuka tabu
Maisha’tafurahia
Nisikilize ghulamu
Wazazi kuwaheshimu
Hilo ni jambo muhimu
Mola kalihimizia
Roho yako iwe Safi
Na laini kama sufi
Mama ‘simwambie uffi
Radhi akakukatia
Na ndugu zako wapende
Usijifanye afande
Kuwapiga kwa makonde
Chuki ukajijengea
Kiunge sana kizazi
Uyajenge na mapenzi
Watu wako uwaenzi
Ni muhimu familia
Haya ukiyafuata
Kweli utametameta
Utangara kama nyota
Katika hini dunia
MWANA
Nimekusikia babu
Hekima yako ajabu
Wala sioni sababu
Maneno kupuuzia
‘Tafuata hima hima
Yote ulioyasema
Nitashika yalo mema
Maovu Kuyakimbia