Iwe juu yenu amani,na za mwenyezi rehema
Mabinti na mabanini, natumai mu wazima
Shukurani kwa mannani,kwa kutupa afya njema
Vyote vikiwa ni vyama, mmumsa imeshika namba
Wino mwingi naujaza,kwenye kikalamu changu
Kuyaacha sitoweza,yaliyo moyoni mwangu
Lazima kuyaeleza,muyajuwe wenzi wangu
Vyote vikiwa ni vyama,mmumsa imeshika namba
Udugu alohimiza, mtume wetu hashimu
Vizuri katueleza,si wa peke yake damu
Ni jambo la kupendeza, kushikana isilamu
Vyote vikiwa ni vyama, mmumsa imeshika namba
La msingi letu lengo,ni kudumisha udugu
Na kuyaziba mapengo,bila kuleta vurugu
Kulisimamisha jengo,la dini ya bwana Mungu
Vyote vikiwa ni vyama, mmumsa imeshika namba
Kinatuleta pamoja,chama hiki kilo aula
Kinatuhimiza waja, kumjua wetu mola
Pia twapata faraja,yakitufika madhila
Vyote vikiwa ni vyama, mmumsa imeshika namba
Imetuunganisha kamba,ilo thabiti na ngumu
Hata ‘kitujia simba,au nyoka mwenye sumu
Au wa majini mamba,kuikata ni vigumu
Vyote vikiwa ni vyama, mmumsa imeshika namba
Pamoja twafurahika,furaha iso kifani
Kila tukijumuika,ni faraja si utani
Ni chama cha kusifika,akibariki mannani
Vyote vikiwa ni vyama, mmumsa imeshika namba
Ni moja yetu kabila,kwa mno twajivunia
Kabila isio ila,ya dini isilamia
Zisizo maana mila,zote twazikatalia
Vyote vikiwa ni vyama,mummsa imeshika namba
Twakuomba Mola wetu,mahabba tuzidishie
Udumu udugu wetu,haja zetu tukidhie
Zote tofauti zetu,shimoni tuzifukie
Vyote vikiwa ni vyama, mmumsa imeshika namba
Tuzidi kushikamana,na ndugu tupendaneni
Huruma kuoneana,kinyongo tuondoeni
Na mikono kushikana,kupelekana peponi
Vyote vikiwa ni vyama, mmumsa imeshika namba.
Nimefikia mwishoni,shukurani Kwa rauf
Kalamu naweka chini,naiweka bila hof
Jina langu ikhiwani, ni Farwa binti Shariff
Vyote vikiwa ni vyama, mmumsa imeshika namba
Farwa hii ni ugwiji na talanta ya hali ya juu. Tafadhali yaendeleze.
Asante