SIO KWA KILA NEEMA TUTANGAZE HADHARANI

Naanza hapa kunadi, umati kuwausia
Namshukuru wadudi, kunipa njema afia
Mada leo ni hasadi, mno tunojitakia
Sio kwa kila neema, tutangaze hadharani

Mwana umejaaliwa, bila shaka ni neema
Kweli umebarikiwa, Leo unaitwa mama
Ila si jambo la Sawa, kuposti  bila kukoma
Sio Kwa kila neema, tutangaze hadharani

Kakujaalia manani, bidii nayo akili
‘mefaulu mtihani, watuma kila mahali
Jamani tuwe makini, hasadi ikae mbali
Sio Kwa kila neema, tutangaze hadharani

Amekuja kwenu mume, harusi tukaicheza
Mbio mithili umeme, wasapu wajitangaza
Na marafiki Kwa shime, pichazo wazisambaza
Sio Kwa kila neema, tutangaze hadharani

Leo umekula kuku, hatutopumua basi
Mapicha huku na huku, waposti tena kwa Kasi
Tuwache uzumbukuku, tutafakari insi
Sio kwa kila neema, tutangaze hadharani

Wapo wanaotamani, kuvipata vyako vyote
Kinyongo ndani Kwa ndani, wanavimezea mate
Ndugu tutahadharini, mabaya yasitukute
Sio kwa kila neema, tutangaze hadharani

1 thought on “SIO KWA KILA NEEMA TUTANGAZE HADHARANI

  1. Hosni

    Nawe umeshasikika, Hasadi jambo hatari
    Usia umeshafika, Waja tutatahadhari
    Pongezi zamiminika, Kwako wewe mshairi
    Umati kuelimika, Bila Shaka hiyo kheri

    Reply

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *