
Damu yanitiririka,ja maji ya mchirizi
Na wala sijakatika,ni mawimbi ya simanzi
Hainitoki mkononi,wala kwenye langu guu
Yamiminika moyoni,kwa yalonifika makuu
Nilikupa wangu moyo,bila shaka bila hofu
Ila roho ulo nayo,umeniachia kovu
‘likuona almasi,unangara kama taa
Kumbe mwenzangu ni fisi,waua bila vifaa
Roho yako ni nyeusi,huna chembe cha huruma
Una mno ubinafsi,ulotenda yaniuma
‘mepata funzo hakika,mapenzi ‘mekuwa sumu
‘mebaki kuhuzunika,kwa sana najihukumu