
Kwa huzuni naandika, jamani shairi hili
Iwe tutafarajika, na kuipata sahali
Kwa jambo lililotuka, tumekuwa mbaya Hali
Ila mola ‘meandika, kuepuka ni muhali
Baada ya kupokea, zilo nzito habari
Huzuni ilienea, kote kote sio Siri
Ajali ilotokea, wengi imewaathiri
Dua tunawaombea, awarehemu qahari
Twakuomba ya manani, aila wape sahali
Ili hunu mtihani, waweze kuuhimili
Subira iwe moyoni, kufuru ikae mbali
Pia watie peponi, kusubiri jambo hili
Pia izidi imani, yao wote familia
Wajue ni mtihani, waweze kuvumilia
Asiwaghuri shetani, kufuruni kuingia
Ni mipango ya mananni, hakika ‘meqadiria
Walio pata ajali, ilahi waghufiria
Wawe kwenye njema hali, kaburini wakingia
Na wayajibu maswali, bila shida kupitia
Wafunike na kivuli, qiyama kikifikia
Tulobaki twainama, ni lini yetu sanati
Mauti ni ya lazima, tuacheni ati ati
Twakuomba ya karima, yawe sahali mauti
Na ifikapo qiyama, ututie jannati
Ibada tumesahau,anasa twaziandama
Mungu tunamdharau,bila ya kurudi nyuma
Twajifanya kusahau,kama kuna na qiyama
Tuzindukeni wadau, ili tupate salama
Kweli kabisa. MwenyeziMungu awaweke pema palio na wema peponi. amin. Asante kwa kutukumbusha kuhusu mauti. Shairi zuriii.
Aaamiin, shukran Sana
Maa shaa Allah. Shairi zuri sana. Allah Awasamehe na sisi tulo nyuma atupe khatima njema
Aaamiin
Shukran Sana